BMT YAPAMBANA KUONGEZA USHIRIKI WA WANAWAKE KATIKA MICHEZO

Baraza la Michezo la Taifa kupitia kwa Mtendaji Mkuu Bi. Neema Msitha limesema litahakikisha linafanya kila linalowezekana katika michezo ya wanawake ili kuongeza mwamko wa ushiriki katika kwa kundi hilo.
Akizungumza tarehe 18 Oktoba, 2023 na Waandishi wa habari, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha la michezo la wanawake na Katibu Mtendaji BMT Bi. Neema Msitha alisema msimu wa tatu (3) wa tamasha hilo litafanyika tarehe 21 katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Mwalimu Julius Nyerere (JNICC)
Alisema watahakikisha wanawekeza katika michezo ya wanawake ambayo imekuwa ikifanya vizuri katika mashindano ya kimataifa.
"Wanawake wamekuwa wakileta heshima kubwa katika taifa letu wanapokwenda katika mashindano ya kimataifa, tumeshuhudia Medali na makombe kutoka katika michezo mbalimbali ikiwemo ya gofu, ngumi na riadha, "alisema.
Msitha aliongeza kuwa tamasha la Tanzanite litaongozwa na Kongamano litakalokuwa na mada adhimu za kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika michezo ikiwemo ya Uongozi na Utawala wa wanawake katika michezo, Mtazamo wa jamii juu ya ushiriki wa wanawake katika michezo pamoja Mchango wa michezo katika ukuaji wa mwanamke kiuchumi.
Vilevile Tamasha litapambwa na mchezo wa karate pamoja na burudani kutoka kwa wasanii wa muziki wa kizazi kipya.
"Sambamba na haya siku hiyo pia tutatoa tuzo kwa wadau wa michezo ambao wameleta heshima kwa taifa, "alisema.